Tuesday, October 8, 2013

Miili 232 imepatikana baada ya boti kuzama karibu na Kisiwa cha Lampedusa eneo la Sicily

Wapiga mbizi nchini Utaliana wamapata idadi kubwa ya maiti katika boti iliyozama na ambayo ilikua imewabeba wahamiaji wa kiafrika kwenda Ulaya siku ya Alhamisi.
Miili 38 iliweza kuondolewa kwenye boti hiyo ambayo wapiga mbizi walikuwa na changamoto kubwa kuweza kuifikia. Idadi rasmi ya waliofariki imesemekana kuwa watu 232.
Wapiga mbizi waliweza kupata watu waliokuwa wamekwama sehemu moja ya boti hiyo kwa mujibu wa maafisa wa huduma za meli akiongeza kuwa ilikuwa imekwama pamoja na kuwapa wakati mgumu kuiondoa miili hiyo.
Boti hiyo ilishika moto na kisha kuzama karibu na kisiwa cha Lampedusa eneo la Sicily.
Manusura wa ajali hiyo iliyotokea umbali wa kilomita moja kutoka ufuoni walikuwa 155.
Juhudi za kuokoa miili kutoka katika boti hiyo zilisitishwa nyakati za usiku lakini zitaanza tena Jumanne
Maelfu ya wahamiaji wa kiafrika hujaribu kufanya safari hatari za majini kutoka Afrika ya Kaskazini hadi katika kisiwa cha Sicily na katika visiwa vingine nchini Utaliana na ajali hutokea mara kwa mara lakini hii ya wiki jana ilikuwa moja ya ajali mbaya zaidi kuwahi kutokea katika safari za wahamiaji kwenda Ulaya.
Mabaki ya meli hiyo yako mita 47 chini ya bahari maana kuwa wapiga mbizi wanaweza kukaa chini ya bahari kwa muda mfupi tu.
Idadi kubwa ya miili imeweza kutolewa kwenye boti hiyo lakini inaaminika kuna miili mingine zaidi ambayo imekwama ndani ya boti.

Taarifa na BBC Swahili

No comments:

Post a Comment